Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Kisukari (Diabetes)


Utangulizi

Unapokula chakula cha wanga kama vile ugali,wali, matoke,mihogo,viazi  n.k hubadilishwa kuwa sukari iitwayo glukozi. Glukozi ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya nishati.Sukari hii hudhibitiwa na homoni iitwayo insulini,inayotolewa na kiungo kinachoitwa kongosho kilichopo katika mfumo wa mmeng'enyo wa chakula. 
 Kisukari ni ugonjwa unaosababisha na mwili kushindwa kubadili glukozi kuwa nishati,hivyo kusababisha kiwango cha sukari kuwa kingi katika mzunguko wa damu.  Kwa lugha ya kitaalamu huitwa Diabetes Mellitus.Kuna aina nyingi za kisukari lakini kwa kurahisisha,kwa leo tutagawanya katika aina kuu tatu.

Aina ya kwanza 

Pia huitwa inslini tegemezi. Kongosho hushambuliwa na magonjwa ya kingamaradhi(autoimmune) na kushindwa kutoa homoni ya insulini. Kisukari cha aina hii humpata mtu akiwa katika umri mdogo. Dawa yake ni mgonjwa kupatiwa insulini.

Aina ya pili

Huu ni ugonjwa wa kurithi. Aina hii huwapata zaidi watu wanene na wanene kupindukia. Watu wanene wana kiasi kikubwa cha matufa mwilini. Mafuta huzuia insulini kubadili sukari kuwa nishati. Aina hii ya kisukari huwapata zaidi watu wazima,ingawa miaka ya hivi karibuni idadi ya vijana wenye aina ya pili ya kisukari wameongezeka duniani kutokana na kuwa wanene, kukosa lishe bora na mazoezi. 

Aina ya tatu

Aina hii huwapata wajawazito. Ujauzito husababisha mabadiliko makubwa ya homoni mwilini ikiwa ni pamoja na kuzuia insulini kufanya kazi. Asilimia 2 hadi 10 ya wanawake hupata kisukari cha aina hii wakati wa ujauzito hasa kuanzia wiki ya 24 na kuendelea. Wengi wao hupona baada ya kujifungua, ingawa wachache hupata aina ya pili ya kisukari wiki au hata miaka kadhaa baada ya kujifungua.


Dalili
  • Kuongezeka kwa hamu ya kula na kiu kupita kiasi,
  • Kupungua uzito ingawa unakula chakula (aina ya kwanza),
  • Mdomo kuwa mkavu,
  • Kukojoa mara kwa mara,
  • Kuchoka kupita kiasi,
  • Kupungua uwezo wa kuona,
  • Vidonda kutokupona haraka,
  • Kukosa hamu ya tendo la ndoa,
  • Kupata maradhi ya njia ya mkojo mara kwa mara kwa wanawake.
Wajawazito wengi hawapati dalili zozote wa kisukari. Mgonjwa hujulikana kutokana na vipimo pale anapoenda kliniki kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Vipimo

Pindi unapokuwa na dalili za kisukari,daktari atakupima kwa kutumia damu kama ifuatavyo ;


 Aina ya kipimo            Kiasi cha kawaida            Kiwango hatarishi           kisukari                          
 Wakati una njaa*

 Chini ya 100 100-125 126 na zaidi
 Wakati umeshiba

 Chini ya 140 140-199 200 na zaidi
 Kipimo cha hemoglobini A1c

 Chini ya %5.7 %5.7-6.4 %6.5 na zaidi
*Ukiwa hujala chakula kwa masaa 10 hadi 12. 


Pindi unapogundulika kuwa una kisukari, daktari atakupa ushauri na kukuanzishia tiba kutokana na aina ya kisukari ulicho nacho.

Vitu vinavyochangia kupata kisukari;
  • Unene,
  • Umri-kadri umri unavyoongezeka una hatari ya kupata kisukari
  • Msongo wa mawazo,
  • Shinikizo la damu,
  • Asili-watu weusi,wahispania na wahindi wana hatari ya kupata kisukari zaidi ya asili zingine.

Madhara ya kisukari

  • Hatari ya kupata magonjwa ya moyo,shinikizo la damu,kiharusi na magonjwa ya mishipa ya damu,
  • Kisukari huharibu mishipa ya fahamu na hivyo kumsababishia mgonjwa kupata ganzi,maumivu na kuhisi miguu kuwaka moto. 
  • Kushambuliwa kwa viungo muhimu kama figo,macho na ubongo. Hivyo kusababisha figo kushindwa kufanya kazi(kidney failure), upofu na mtindio wa ubongo.
  • Vidonda kutokupona
  • Kupata magonjwa ya ngozi na njia ya mkojo.


Kinga

Ingawa aina ya pili ya kisukari ni ugonjwa wa kurithi,kuna baadhi ya hatua ambazo zikichukuliwa humsaidia mtu kuepuka kupata au kupunguza uwezekano wa kupata ugonjwa huu;

  • Epuka kula vyakula vya mafuta kupita kiasi,
  • Fanya mazoezi kuzuia kunenepa,
  • Epuka msongo wa mawazo,
  • Punguza au epuka kunywa pombe,
  • Epuka uvutaji wa sigara,
  • Lala usingizi wa kutosha.







Tiba

Tiba dhidi ya kisukari hupangiliwa kutokana na aina ya kisukari, kiwango cha sukari na umri wa mgonjwa.
Kwa ufupi aina ya kwanza ya kisukari dawa yake ni inslini na aina ya pili na tatu ya kisukari ni dawa ambazo husaidia insulini kupenya katika tishu na kuongeza nguvu ya insulini kufanya kazi. 


Hitimisho

Kisukari ni ugonjwa unaozuilika,cha kufanya ni kuepuka hulka hatarishi na kufuata maelekezo ya wataalamu  wa afya. Lakini ikumbukwe kuwa siku zote kinga ni bora kuliko tiba. 










Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ualbino (Albinism)

 Ualbino ni nini? Ualbino ( albinism ) ni hali ya kiafya inayotokana na mwili kukosa uwezo wa kutoa homoni aina ya melanin . Homoni hii pamoja na kazi nyingine inahusika na utoaji wa rangi ya mwili. Ukosefu wa melanin huathiri ngozi, macho na nywele.  Ualbino ni hali ya kurithi kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Ikumbukwe kuwa  Albino sio mgonjwa bali ni mlemavu wa macho, nywele na ngozi ambavyo huathiri maisha yake ya kila siku, hata kufupisha umri wa kuishi. Nje na binadamu ualbino unaathiri pia wanyama, samaki, wadudu, nyoka, mijusi, ndege na hata mimea (kwa mimea hutokana na ukosefu wa klorofili).  Waathiriwa wenyewe nchini Tanzania waliamua kupendelea kuitwa "watu wenye ualbino" kutokana na matumizi mabaya ya neno zeruzeru katika utamaduni wa Afrika ya Mashariki ambako watu mara nyingi waliona uhusiano kati ya waathiriwa na mapepo au mizimu. Kuenea kwa Ualbino Tafiti zinaonyesha kuwa mtu mmoja kati ya 20,000 duniani ni albino, lakini kwa sababu zisizofahamika ba...

Ugonjwa wa Fistula ( Rectovaginal Fistula)

  Fistula ni nini? Fistula ni tundu lisilo la kawaida ambalo hutokana na kuungana kwa sehemu ya chini ya utumbo mpana (njia ya haja kubwa) na njia ya mkojo au njia ya uke, hivyo kumfanya mgonjwa kushindwa kuzuia haja au kutokwa na hajak ubwa ukeni.  Mara nyingi husababishwa na kujeruhiwa kwa sehemu hizo wakati wa kujifungua hasa kwa wanawake wanaozaa katika umri mdogo au wanaokosa msaada stahiki wakati wa kuzaa. Kwa mujibu wa shirika la afya duniani,  inakadiriwa kuwa wanawake zaidi ya milioni mbili kutoka Afrika na Asia wanaishi na ugonjwa huu, bila kupatiwa matibabu yoyote, kwa upande wa Tanzania wengi wamekua wakitafuta msaada kwa waganga wa jadi.   Nini Husababisha Fistula? Ugonjwa wa Fistula unaweza kusababishwa na mambo kadhaa ikiwemo yafuatayo; Majeraha wakati wa kujifungua, Maambukizi ya Mfumo wa uzazi (PID), Mgonjwa ya utumbo mpana kama vile Crohn , Saratani ya mfumo wa uzazi au utumbo mpana, Majeraha yanayotokana na ajali au upasuaji wa sehemu ya nyonga. Fi...

Homa ya Mfumo wa Uzazi (Pelvic Inflamatory Disease- PID )

Homa ya Mfuko wa Uzazi ni nini? Ni magonjwa yanayompata mwanamke katika uke, shingo ya uzazi,mfuko wa uzazi, mirija ya uzazi na sehemu inayozunguka mfumo wa uzazi. Karibu asilimia 85 ya watu wanaopata homa hii hutokana na magonjwa yanayoambukizwa kwa njia ya kujamiiana, wengi wao wakiwa na vimelea vya bakteria kama vile  kisonono (gonorrhoea) , kaswende (syphilis) , klamidya n.k. Wakati mwingine mgonjwa hupata homa hii kutokana na bakteria ambao kawaida huwa wapo mwilini na hawana madhara lakini kwa sababu mbalimbali kama kupungua kwa kinga, kisukari, saratani, upasuaji, kuwa na magonjwa ya mfumo wa chakula n.k wanasababisha homa.   Dalili Maumivu makali chini ya kitovu na kiunoni, Maumivu wakati wa tendo la ndoa, Maumivu wakati wa kukojoa, Maumivu makali au kutokwa na damu nyingi wakati wa hedhi, Kutokwa na majimaji yenye harufu kali  na rangi ya njano, kijani au kahawia ukeni, Kuwa na homa jotoridi 38.3 au zaidi, Kujisikia uchovu, kichefuchefu n.k.   Sababu Homa ya...