Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Homa ya Mfumo wa Uzazi (Pelvic Inflamatory Disease- PID )



Homa ya Mfuko wa Uzazi ni nini?



Ni magonjwa yanayompata mwanamke katika uke, shingo ya uzazi,mfuko wa uzazi, mirija ya uzazi na sehemu inayozunguka mfumo wa uzazi.

Karibu asilimia 85 ya watu wanaopata homa hii hutokana na magonjwa yanayoambukizwa kwa njia ya kujamiiana, wengi wao wakiwa na vimelea vya bakteria kama vile  kisonono (gonorrhoea), kaswende (syphilis), klamidya n.k.

Wakati mwingine mgonjwa hupata homa hii kutokana na bakteria ambao kawaida huwa wapo mwilini na hawana madhara lakini kwa sababu mbalimbali kama kupungua kwa kinga, kisukari, saratani, upasuaji, kuwa na magonjwa ya mfumo wa chakula n.k wanasababisha homa.

 

Dalili




  • Maumivu makali chini ya kitovu na kiunoni,
  • Maumivu wakati wa tendo la ndoa,
  • Maumivu wakati wa kukojoa,
  • Maumivu makali au kutokwa na damu nyingi wakati wa hedhi,
  • Kutokwa na majimaji yenye harufu kali  na rangi ya njano, kijani au kahawia ukeni,
  • Kuwa na homa jotoridi 38.3 au zaidi,
  • Kujisikia uchovu, kichefuchefu n.k.

 

Sababu

Homa ya mfumo wa uzazi mara nyingi husababishwa na vimelea vya bakteria wanaambukizwa kwa njia ya tendo la ndoa (sexually transmitted diseases -STD) kama vile;

  • Kisonono (Neisseria gonorrhoeae),
  • Kaswende (Treponema pallidum),
  • Klamidya (Chlamydia trachomatis ) n.k

Au kwa asilimia chache husababishwa na vimelea wasioambukizwa kwa njia ya ngono.

 

Nani yupo hatarini kupata homa hii?

Kila mwanamke ambaye yupo kwenye umri wa kuzaa anaweza kupata homa ya mfumo wa uzazi lakini kuna hali au vitendo vinavyosababisha urahisi wa maambukizi kama vile;

  • Kuwa na mpenzi zaidi ya mmoja,
  • Kufanya ngono zembe bila kutumia kinga,


  • Kuwa na mpenzi mpya,
  • Kama ulishawahi kupata homa hii au magonjwa ya aina hii kabla,
  • Kushiriki ngono katika umri mdogo,
  • Kama una umri wa chini ya miaka 25,
  • Kama ulishawahi kufanyiwa upasuaji kwenye mfumo wa uzazi au mfumo wa mmeng’enyo wa chakula,
  • Kama una vifaa vya kuzuia mimba kwenye mfuko wa uzazi ( intrauterin device ),


  • Kutoa mimba kiholela bila kuzingatia hatua za kiafya au kupata mimba nje ya mfuko wa uzazi (ectopic pregnancy ),
  • Kupata ajali n.k.

Wakati mwingine homa ya mfumo wa uzazi inaweza kumpata mgonjwa siku, wiki, miezi au miaka mingi baada ya kushiriki tendo la ndoa. Hivyo sio busara kuanza kushutumiana usaliti n.k

 


Uchunguzi

Ni muhimu sana ukipata dalili hizo hapo juu kwenda kwenye kituo cha afya kwa uchunguzi zaidi. Kupuuzia kufanya hivyo vinaweza kumhatarishia maisha mgonjwa, kwani homa hii inaweza kuenea mwili mzima kwa njia ya mfumo wa damu ( sepsis). 

 Kuwahi kufanyiwa uchunguzi pia kutampunguzia maumivu, kupata tiba kwa wakati na kutaepusha madhara ya baadae kama ulemavu wa kudumu, utasa au hata kifo.

Mtaalamu wa afya atamuuliza  mgonjwa vitu mbalimbali kama historia ya mapenzi, wapenzi, magonjwa mengine, umri n.k hivyo ni vyema kutoa taarifa zisizopotosha ili kuweza kupatiwa huduma zilizo sahihi. 

Kwa wale  wenye wapenzi ni muhimu kufanyiwa uchunguzi na kupata matibabu ya pamoja ili kuondoa tatizo la kujirudia rudia.

Mtaalamu wa afya atamfanyia mgonjwa uchunguzi wa kina kama vile mkojo, damu,  kupima mimba na kuchukua sampuli (swab). 

Wakati mwingine vipimo vingine kama ultrasound vinaweza kutumiwa ili kuangalia ukubwa wa tatizo na kuangalia uwezekano wa kuwepo magonjwa mengine kama vile homa ya kidoletumbo (appendicitis), homa ya ukuta wa tumbo (peritonitis) n.k.

 

Tiba

Baada ya uchunguzi, daktari atamwanzishia mgonjwa dawa (antibiotics) zenye uwezo wa kuua bakteria zaidi ya mmoja  au mchanganyiko wa antibiotics zaidi ya moja haraka iwezekanavyo wakati majibu ya sampuli yakisubiriwa.



 Ni muhimu daktari kupewa taarifa kama mgonjwa ana wasiwasi wa mimba kwani kuna dawa zisizofaa kupewa mjamzito. Kawaida mgonjwa hupewa dawa hizi kwa muda wa wiki mbili, kisha kufanyiwa uchunguzi baada ya hapo ili kuamua kuendelea au kusitisha matibabu.

 Wakati huo huo mgonjwa atapewa dawa za maumivu na kushauriwa kula mlo kamili na kunywa maji mengi. Wakati matibabu yakiendelea, haishauriwi kufanya tendo la ndoa.

Wakati mwingine mgonjwa anaweza kulazwa hospitalini kwa uangalizi wa karibu na kupewa dawa kwa njia ya mishipa ya damu (İ.V) kama yu mahututi, au kama anashindwa kula na kunywa au endapo daktari atakuwa na wasiwasi wa huduma ya mgonjwa akiwa nyumbani.

 

Nini kifanyike ili kuepuka homa hii?

Kwa kuwa homa hii inaweza kumsababishia mgonjwa madhara ( complications) ya muda mrefu au ya kudumu kama vile; utasa,  homa kujirudia rudia, mimba za nje ya mfuko wa uzazi n.k, ni vyema kujiepusha na tabia hatarishi kama ifuatavyo;

  • Epuka ngono zembe,
  • Epuka kuwa na wapenzi zaidi ya mmoja,
  • Epuka kufanya tendo la ndoa wakati wahedhi,
  • Tumia kinga ili kuepuka maradhi,
  • Jenga tabia ya kupima afya yako na mpenzi wako pale unapokuwa na dalili yoyote,
  • Epuka kutumia dawa bila ushauri wa daktari,
  • Epuka tabia hatarishi kama ulevi kupindukia, madawa ya kulevya yanayochochea vitendo vya ubakaji.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ualbino (Albinism)

 Ualbino ni nini? Ualbino ( albinism ) ni hali ya kiafya inayotokana na mwili kukosa uwezo wa kutoa homoni aina ya melanin . Homoni hii pamoja na kazi nyingine inahusika na utoaji wa rangi ya mwili. Ukosefu wa melanin huathiri ngozi, macho na nywele.  Ualbino ni hali ya kurithi kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Ikumbukwe kuwa  Albino sio mgonjwa bali ni mlemavu wa macho, nywele na ngozi ambavyo huathiri maisha yake ya kila siku, hata kufupisha umri wa kuishi. Nje na binadamu ualbino unaathiri pia wanyama, samaki, wadudu, nyoka, mijusi, ndege na hata mimea (kwa mimea hutokana na ukosefu wa klorofili).  Waathiriwa wenyewe nchini Tanzania waliamua kupendelea kuitwa "watu wenye ualbino" kutokana na matumizi mabaya ya neno zeruzeru katika utamaduni wa Afrika ya Mashariki ambako watu mara nyingi waliona uhusiano kati ya waathiriwa na mapepo au mizimu. Kuenea kwa Ualbino Tafiti zinaonyesha kuwa mtu mmoja kati ya 20,000 duniani ni albino, lakini kwa sababu zisizofahamika ba...

Ugonjwa wa Fistula ( Rectovaginal Fistula)

  Fistula ni nini? Fistula ni tundu lisilo la kawaida ambalo hutokana na kuungana kwa sehemu ya chini ya utumbo mpana (njia ya haja kubwa) na njia ya mkojo au njia ya uke, hivyo kumfanya mgonjwa kushindwa kuzuia haja au kutokwa na hajak ubwa ukeni.  Mara nyingi husababishwa na kujeruhiwa kwa sehemu hizo wakati wa kujifungua hasa kwa wanawake wanaozaa katika umri mdogo au wanaokosa msaada stahiki wakati wa kuzaa. Kwa mujibu wa shirika la afya duniani,  inakadiriwa kuwa wanawake zaidi ya milioni mbili kutoka Afrika na Asia wanaishi na ugonjwa huu, bila kupatiwa matibabu yoyote, kwa upande wa Tanzania wengi wamekua wakitafuta msaada kwa waganga wa jadi.   Nini Husababisha Fistula? Ugonjwa wa Fistula unaweza kusababishwa na mambo kadhaa ikiwemo yafuatayo; Majeraha wakati wa kujifungua, Maambukizi ya Mfumo wa uzazi (PID), Mgonjwa ya utumbo mpana kama vile Crohn , Saratani ya mfumo wa uzazi au utumbo mpana, Majeraha yanayotokana na ajali au upasuaji wa sehemu ya nyonga. Fi...