Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Ualbino (Albinism)


 Ualbino ni nini?

Ualbino (albinism) ni hali ya kiafya inayotokana na mwili kukosa uwezo wa kutoa homoni aina ya melanin. Homoni hii pamoja na kazi nyingine inahusika na utoaji wa rangi ya mwili. Ukosefu wa melanin huathiri ngozi, macho na nywele. 




Ualbino ni hali ya kurithi kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Ikumbukwe kuwa  Albino sio mgonjwa bali ni mlemavu wa macho, nywele na ngozi ambavyo huathiri maisha yake ya kila siku, hata kufupisha umri wa kuishi. Nje na binadamu ualbino unaathiri pia wanyama, samaki, wadudu, nyoka, mijusi, ndege na hata mimea (kwa mimea hutokana na ukosefu wa klorofili). 






Waathiriwa wenyewe nchini Tanzania waliamua kupendelea kuitwa "watu wenye ualbino" kutokana na matumizi mabaya ya neno zeruzeru katika utamaduni wa Afrika ya Mashariki ambako watu mara nyingi waliona uhusiano kati ya waathiriwa na mapepo au mizimu.

Kuenea kwa Ualbino

Tafiti zinaonyesha kuwa mtu mmoja kati ya 20,000 duniani ni albino, lakini kwa sababu zisizofahamika barani Afrika, kusini mwa jangwa la Sahara kuna idadi kubwa zaidi ya albino kuliko kokote duniani. Kwa mfano inasadikiwa kwa nchini Tanzania kuna albino mmoja kwa kila watu 1,400. Nchi ya Zimbabwe inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa zaidi, ikiwa na albino mmoja kwa kila watu 1,000. 

Asili

Albino huzaliwa na hali ya kukosa uwezo wa kujenga homoni ya melanin ambayo ni muhimu kama kinga dhidi ya mionzi ya jua. Watu wenye ualbino huwa na nywele nyeupe au njano, na ngozi nyeupe. Macho yao ni bluu au hata pinki.
Uwezo wa kutengeneza homoni au pigimenti ya melanin hutegemea vinasaba (genes) vya kurithi. Vinasaba hivi vikiwa vibovu ndio husababisha mwili kushindwa kutoa melanin. 
Ikumbukwe kuwa vinasaba  hivi vibovu hubebwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Kwa kuwa vinasaba hivi vinatoka kwa baba na mama, inamaanisha kwamba mtu huzaliwa albino kama wazazi wote wawili tayari wana vinasaba vibovu. Wazazi hao wote wanaweza kuwa ni wabebaji tu na sio albino. Watoto wengine pia wanaweza kuwa sio albino. Hali hii inaendelea katika familia na inaweza kuonekana mara kwa mara inategemea na kupatikana kwa vinasaba  husika katika wazazi wote wawili.


Dalili

Ni rahisi kumtambua albino kutokana na ngozi  na nywele  zake kuwa nyeupe kuliko kawaida. 
  • Kupata majeraha kirahisi na pia kuchelewa kupona, 
  • Kupata majeraha baada ya kukaa muda mrefu juani,
  • Kuwa ma mabaka meusi ambayo hutokwa na damu kirahisi, 
  • Nywele nyeupe, nyekundu au kahawia,
  • Macho ya bluu au pinki.

Kutokana na macho kushindwa kuchuja mwanga wa jua kwa kukosekana au upungufu  wa melanin kwenye mboni, hali hii huathiri sana uwezo wake wa kuona. Vilevile hushindwa kutambua ukaribu au umbali wa kitu na kutofautisha rangi. Hii inaweza kuwa hatari hasa kwa magari na taa za barabarani.


Tiba

Kwa bahati mbaya ualbino ni hali isiyotibika. Tiba yake hulenga zaidi kwenye vitu au hatua zinazochukuliwa ili kuboresha maisha yake kama vile kuona na kinga dhidi ya jua au majeraha. 

Mambo kadha kama yafuatayo yanaweza kufanywa;
  • kufanyiwa vipimo vya macho mara kwa mara na kupatiwa miwani maalumu inayorekebisha kuona na kupunguza mwanga.
  • kufanyiwa vipimo vya ngozi kila mwaka ili kutibu majeraha pamoja na kugundua endapo kuna madoa yanayoweza kuwa na tabia ya saratani ya ngozi kutokana na mionzi mikali ya jua.



Albino anaweza kufanya yafuatayo ili kujilinda yeye mwenyewe;
  • Kuvaa miwani ya jua (sunglasses),
  • Kuvaa nguo zinazoakisi mwanga na kumlinda kutokana na mionzi,
  • Kupaka mafuta malumu yaliyotengenezwa kwa ajili ya  kupunguza athari za mionzi ya jua,
  • Kuepuka tabia hatarishi kama vile ulevi, mihadarati, ugomvi n.k,
  • Kupunguza kutoka nje wakati wa jua kali au kutumia kofia pana au mwamvuli.


Kwa wanafunzi hasa wa shule za msingi, ni muhimu walimu kuwaelimisha wanafunzi wenzake juu ya hali ya albino ili kushirikiana nae katika kuboresha maisha yake.

Hatua zingine ni kama vile;
  • kuepuka unyanyapaa,
  • kukaa dawati la mbele,


  • mwalimu kuandika kwa maandishi makubwa,
  • kutumia daftari lenye rangi iliyofubaa ili kupungua kuakisi mwanga, pia kuepuka kutumia rangi mbalimbali katika maandishi,
  • kuweka mapazia darasani na kupunguza mwanga( taa za umeme za kwenye dari),
  • kumpa muda zaidi hasa wakati wa mtihani.

Hitimisho

Kwa bahati mbaya katika jamii nyingi hasa katika bara la Afrika kumekuwa na imani duni za kishenzi zinazohusisha ualbino na mapepo, mizimu au ushirikina. Hapa kwetu Tanzania, Burundi n.k kumekuwa na imani potofu kuwa viungo vya albino vinaleta bahati kama vile mali, hivyo kusababisha mauaji ya kikatili yasiyokubalika ya albino. Ni changamoto ya kila binadamu kutoa elimu sahihi juu ya suala hili ili kulinda maisha wa wenzetu wasio na hatia. 












Maoni

  1. Asante sana kwa makala nzuri Daktari bila shaka tunaruhusiwa kushare na wengine keep it up

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Msongo wa Mawazo (Depression)

Msongo wa mawazo ni nini? Msongo wa mawazo  ( Depression ) ni mfadhaiko wa akili anaoupata mtu kutokana na shida, taabu, dhiki, matatizo au changamoto zinazomkabili katika maisha ya kila siku. Msongo wa mawazo hutokana na pale mtu anaposhindwa kukabiliana na jambo linalomtatiza. Msongo wa mawazo huwapata watu wa rika na asili zote. Tafiti zinaonyesha kuwa wanawake  hupata msongo wa  mawazo zaidi kuliko wanaume. Msongo wa mawazo ni tatizo la kimwili pamoja na kiakili. Dalili. kujisikia maumivu sehemu mbalimbali za mwili hasa kichwa, kukosa hamu ya kula au kula chakula kupitiliza,hasa vyakula vyenye madhara, kukosa hamu ya tendo la ndoa, kuwa na huzuni wakati wote na kujisikia mnyonge, kusahau kirahisi au kupungua kwa uwezo wa kufikiria, kujisikia mpweke au kukosa matumaini ya maisha, kupungua kwa uwezo wa kimasomo kwa wanafunzi, kuwa na hofu au kutokujiamini, kupungua au kuongezeka uzito bila kupenda, kushindwa kulala au kulala kupindukia, kukosa utulivu w...

Homa ya Findofindo (Tonsillitis)

Utangulizi   Findofindo ( Tonsillitis) ni nini?  Mafindofindo ni mashambulizi ya virusi au bakteria kwenye tezi za koo zijulikanazo kama findo. Asilimia 15 mpaka 30 ya mashambulizi haya yanatokana na bakteria ila asilimia kubwa hutokana na virusi.  Dalili za mafindofindo   Kwa kawaida ni ngumu kutofautisha kati ya maambukizi yatokanayo na bakteria na yale ya virusi ila leo nitakujuza siri ndogo. Zipo dalili za pamoja na zile za tofauti.  Zifuatazo ni dalili za pamoja za mafindofindo unazoweza kuzipata kwa wagonjwa waliopata maambukizi ya bakteria na yale virusi  Maumivu ya koo Kupata shida katika kumeza  Homa kali ( Zaidi ya nyuzi joto 38 za sentigredi)  Maumivu ya kichwa  Maumivu ya sikio  Utando katika findo Dalili zifuatazo zinaasilimia kubwa sana kupatikana kwa mtu mwenye mashambulio yatokanayo na virusi.  Homa ( zaidi ya nyuzi joto 38 za sentigredi)   Uvimbe shingoni ( upande mmoja au pande mbili)   Maumivu...